Monday, January 7, 2019

Waziri Mkuu atoa uamuzi sakata la mawaziri wawili, RC

 


Dodoma. Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amezitaka kampuni zote zinazosambaza nguzo za umeme kulipa ushuru wa asilimia tano kwa kila nguzo kwa halmashauri wanakotoa nguzo hizo kama ilivyoelekezwa na Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa.
Alitoa uamuzi huo jana mjini Dodoma ikiwa zimepita siku mbili tangu alipowataka Waziri wa Nishati, Dk Medard Kalemani; Waziri wa Tamisemi, Selemani Jafo na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Ally Hapi kufika ofisini kwake mjini hapa, ili wamweleze sababu zinazofanya nguzo za umeme kuzuiwa zisitoke kwenye halmashauri ikiwamo ya Mufindi.
Wito huo uliwahusu pia wakuu wa wilaya, wenyeviti na wakurugenzi wa halmashauri zilizozuia nguzo hizo kusafirishwa.
Akiwa katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Kijiji cha Nyoni wilayani Mbinga mkoani Ruvuma, Jumamosi iliyopita, Majaliwa alisema ni jambo la ajabu wananchi kukosa umeme kutokana na ukosefu wa nguzo wakati zipo, lakini zinazuiwa na watu wachache kwa masilahi yao.
Jana, katika taarifa iliyotolewa na ofisi yake, alisema ameagiza ushuru ulipwe baada ya kupata taarifa kuhusu kampuni ya New Forest ambayo ina mkataba na Shirika la Umeme (Tanesco) wa kusambaza nguzo za umeme.
Alisema kwa muda mrefu kampuni hiyo imekuwa ikikaidi kulipa ushuru wa asilimia tano ya gharama ya kila nguzo na kusababisha ufike Sh2.9 bilioni, jambo lililoufanya uongozi wa Mkoa wa Iringa kuzuia nguzo hizo zisitoke.
Baada ya kupata maelezo hayo, alimuagiza Hapi kuiandikia madai kampuni hiyo ili ilipe ushuru huo kuanzia Julai 2018 walipoanza kusambaza nguzo.
Viongozi wengine waliohudhuria kikao hicho ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Jenista Mhagama; Waziri wa Nishati, Dk Medard Kalemani; Naibu Waziri Tamisemi, Josephat Kandege; Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Ashatu Kijaji; Naibu Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Stella Manyanya pamoja na maofisa wengine wa Serikali.



No comments:

Post a Comment