Wednesday, January 16, 2019

CCM waunga mkono marekebisho muswada vyama vya siasa

Katibu wa Halmashauri Kuu Itikadi na Uenezi

Katibu wa Halmashauri Kuu Itikadi na Uenezi Humphrey PolePole akizungumza wakati wa mkutano wa kutoa maoni ya mabadiliko ya muswada wa sheria ya vyama vya Siasa  unaofanyika jijini, Dar es Salaam leo. 
Dar es Salaam. Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Humphrey Polepole amesema chama hicho tawala kinaunga mkono utoaji wa maoni ya muswada wa vyama vya siasa wa mwaka 2018.
Amesema sheria inayotumika sasa ina mapungufu mengi yanayopaswa kurekebishwa kulingana na mazingira yaliyopo nchini.
Akizungumza leo Jumatano Januari 16, 2019 kwenye mkutano wa utoaji maoni ya wanachama wa CCM kuhusu muswada huo, Polepole amesema si kweli kwamba muswada huo umetoa madaraka makubwa kwa msajili wa vyama vya siasa.
“Msajili anatakiwa awe huru kuhoji kuhusu vyama vyetu ikiwamo vikao vilivyoketi kupitisha wagombea, kwa sasa mamlaka hayo hana na atapata ikiwa muswada huu utapitishwa kuwa sheria,” amesema Polepole.
Amesema mswada huo unasimamia kuona vyama vya siasa vinajiwekea mfumo thabiti wa demokrasia ndani ya vyama vyao ikiwamo namna ya kupata viongozi na uwazi kwenye mapato na matumizi ya fedha.
“CCM tunasema tunataka kuwa na sheria itakayosaidia vyama vya siasa kuwa makini na kutofanya mchezo yanapokuja masuala ya kuwajibika,” amesema.
Polepole amesema wanaunga hoja kuwa msajili awe na mamlaka ya kufuatilia vyama vya siasa vyenye usajili wa kudumu.
“Apite kuuliza jamani vipi mmefanya uchaguzi? Mwenyekiti wenu amechaguliwa? Tunataka aje kuuliza kwa sababu sheria ya awali inayotumika sasa haikumpa mamlaka hayo,” amesema.
Awali katibu wa siasa na mahusiano ya kimataifa wa CCM, Kanali Mstaafu Ngemela Lubinga amewataka wanachana wa chama hicho kutoa maoni yao bila wasiwasi kuhusu muswada huo.
Amesema kusudi kubwa la muswada huo ni kutengeneza mazingira ya kuwaongoza Watanzania kulingana na mazingira yaliyopo.
Amesema muswada huo unapiga marufuku kuanzishwa kwa vikundi vya ulinzi na usalama ndani ya vyama vya siasa jambo ambalo ni sahihi. “Kwa hiyo niseme tu muswada huu ni njia ya demokrasia, tumepewa haki ya kujadili,” amesema.

No comments:

Post a Comment