
Rais john magufuli amesema kama kuna changamoto ambazo bado hazijafanyiwa kazi na uongozi wake hana uhakika kama kiongozi atakayekuja atakuwa na uwezo wa kuzitatua na kufafanua kuwa safari ya kutatua changamoto ina magumu mengi.
Magufuli ameyasema hayo leo Ijumaa Januari 18, 2019 katika hafla ya makabidhiano ya mfumo wa kusimamia uwazi katika mawasiliano ya simu (TTMS) wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA).
Amesema katika safari ya kutatua changamoto anakutana na magumu mengi na ndiyo maana amekuwa akihitaji nguvu za Mungu kutekeleza majukumu yake.
“Viongozi wa dini endeleeni kuliweka Taifa hili kwenye mikono ya Mungu. Hii ni vita kama ilivyo nyingine na vita ya uchumi inahitaji maombi sana, bila maombi kazi hii haiwezi kufanyika,” amesema.
“Hao wanaokaa gizani hauwezi kujua ana kisu, ana panga au ameweka nyoka mfukoni lakini huko gizani huwa wanatolewa kwa maombi, yatawapumbaza huko gizani wasitake kufanya walichokusudia.”
Amesema kufanya hivyo kutawafanya viongozi wa nchi kusimamia misingi ya uadilifu na upendo wa kweli katika kulitumikia Taifa tajiri, lenye changamoto nyingi zinazohitaji kutatuliwa.
No comments:
Post a Comment