Tuesday, November 5, 2019

Bunge la Tanzania sasa kidigitali zaidi

Spika wa Bunge Job Ndugaia,akionyesha Tablet

Dodoma. Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai amezitaka taasisi zote zinazotaka kutoa semina kwa wabunge, wajiandae kuzitoa kwa njia ya mtandao kwa kuwa wabunge wako mtandaoni.
Spika Ndugai ametoa kauli hiyo leo Jumanne Novemba 5, 2019 katika kikao cha kwanza cha mkutano wa 17 katika Bunge la 11.
Kiongozi huyo amesema Bunge limepiga hatua kwa kuwa na teknolojia ya kisasa zaidi kwa kuwa na mitandao ya pamoja na vifaa vya kisasa.
“Lakini nawaomba na taasisi zingine kuiga mfano wa bunge kwa kuja na teknolojia ya kisasa ili kupunguza Makaratasi, lakini taasisi zinazotaka kutoa semina kwa wabunge wajipange katika teknolojia hii,” amesema Ndugai.
Wabunge wote leo waliingia na vifaa vya kisasa thabiti na kila kitu kimetumwa humo, hivyo wabunge walikuwa wakifuatilia kwa njia ya mtandao.
Hata hivyo, Mawaziri walikuwa wakijibu maswali ya wabunge kwa kutumia karatasi za majibu badala ya kusoma kwenye tabiti (tablet) zao.

Friday, September 13, 2019

Rais Magufuli kufungua mkutano wa wakuu wa polisi Afrika mashariki



Rais wa Tanzania, John Magufuli


 Rais wa Tanzania, John Magufuli anatarajiwa kufungua mkutano mkuu wa 21 wa shirikisho la wakuu wa polisi wa nchi za  Afrika Mashariki Septemba 19, 2019 jijini Arusha.
Mkutano huo utashirikisha wajumbe ambao ni ma Inspekta Jenerali wa Polisi kutoka nchi 14 za  Burundi, Comorro,Djibout , Congo, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Eritrea, Ethiopia, Kenya, Rwanda, Shelisheli, Sudan Kusini, Sudan, Uganda na mwenyeji Tanzania.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Arusha nchini Tanzania leo Ijumaa, Septemba 13,2019, Msemaji wa Jeshi la Polisi la Tanzania, David Misime amesema maandalizi yote ya mkutano yamekamilika na wanaanza kupokea wageni  kuanzia leo.
Misime amesema kabla ya ufunguzi wa mkutano huo kutakuwa na vikao vya wakuu wa vitengo vya Interpol utakaofanyika kati ya Septemba 15 hadi  17,2019 kisha kufuatiwa na mkutano wa wakurugenzi wa upelelezi wa makosa ya jinai (DCI) na kikao cha wajumbe wa kamati ndogo ya mafunzo.
 Amesema kutakuwa na kikao cha kamati ndogo ya wataalamu wa sheria, vikao vya wajumbe wa kamati ya dawati la maswala ya unyanyasaji wa kijinsia pamoja na kikao cha  wajumbe wa masuala ya kukabiliana na ugaidi nchini.
Misime amesema mkutano huo utakaokuwa na kauli mbiu ya "Kuimarisha ushirikiano na ubunifu katika kupambana na uhalifu unaovuka mipaka"  ukiwa na  lengo la kuongeza ushirikiano katika kukabiliana na makosa yanayovuka mipaka na kuweka mikakati ya pamoja katika maazimio ya kukabiliana na uhalifu wa kuvuka mipaka.
“Katika mkutano huu, Inspekta Jenerali wa Polisi wa Tanzania  Simon Sirro atakabidhiwa uenyekiti wa shirikisho la wakuu wa polisi wa nchi za Afrika Mashariki,” amesema Misime.
Amesema katika mkutano huo, watatenga siku moja ya kuwapeleka wageni hao katika Chuo cha Mafunzo ya Polisi Moshi (CCP) mkoani Kilimanjaro kuangalia madarasa na mabweni mapya yaliyojengwa na Serikali na wadau ili kuleta wanafunzi wao wa polisi kujifunza.

UDSM wamuomba Magufuli kuingilia kati vurugu Afrika kusini


Dar es Salaam. Serikali ya Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (Daruso) nchini Tanzania kimelaani vikali mashambulio ya kibaguzi yaliyotokea nchini Afrika Kusini kwa watu wa mataifa mengine ya Afrika  huku wakimtaka Rais wa Tanzania, John Magufuli ambaye ni Mwenyekiti mpya wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (Sadc) kuingilia kati mzozo huo.

Taarifa iliyotolewa jana Alhamisi Septemba 12,2019 na Waziri wa Habari, Mawasiliano wa Daruso, Judith Mariki iliwaomba viongozi wa Afrika kukutana na kutumia maarifa na busara ili kudhibiti vitendo hivyo ambavyo ni kinyume cha maadili, mila na ubinadamu.
“Tunatoa wito kwa Rais wa Tanzania, John Magufuli ambaye ni Mwenyekiti wa Sadc, kuitisha mkutano wa dharura ili ujadili na viongozi wenzake kujadili mwafaka wa hali hiyo, ili kuwaleta pamoja kwa amani, kabla hali haijawa mbaya zaidi isipodhibitika,” alisema Mariki.
Alisema matukio hayo ya kinyama yanaharibu umoja na mshikamano wa Kiafrika kwa kuwa Waafrika wamekuwa wakiishi kama ndugu na kwa amani tangu wakati wa mapambano ya uhuru.
“Tusiruhusu mgawanyiko kutokana na tofauti zetu kwa sababu tunatokea nyumba moja kwa nini tugombee kipande cha mkate? Tunatoka bara moja kwa nini tuwadhalilishe ndugu zetu? Waafrika ni ndugu, ni walinzi wa ndugu zetu, mwafrika hawezi kuwa mgeni kwenye ardhi ya Afrika. Acha ubaguzi Afrika,” alisema Mariki.
Aliongeza, “Afrika ni kwa ajili ya Waafrika, tuache kuuana wenyewe kwa wenyewe kwa sababu tokea Afrika, umoja hautashindwa. Mungu ibariki Afrika, Mungu wabariki Waafrika.”

Thursday, September 12, 2019

Rais Magufuli afanya uteuzi, mkurugenzi mkuu usalama wa taifa

Rais wa Tanzania, John Magufuli,Dk Modestus Kipilimba,Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa kuchukua nafasi ya Dk Modestus Kipilimba

Dar es Salaam. Rais wa Tanzania, John Magufuli amemteua na kumuapisha Diwani Athuman kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa kuchukua nafasi ya Dk Modestus Kipilimba.
Taarifa iliyotolewa leo Alhamisi Septemba 12, 2019 na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Gerson Msigwa inaeleza kuwa uteuzi wake umeanza leo.
Kabla ya uteuzi huo,  Diwani aliyeapishwa Ikulu, Dar es Salaam leo alikuwa mkurugenzi mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru).
Akizungumza baada ya kumuapisha, Rais Magufuli amemtaka kuchapa  kazi kwa juhudi na maarifa na kuweka mbele maslahi ya Taifa.

Wednesday, September 11, 2019

Rais Magufuri afanya uteuzi bodi ya LATRA,TFRA


Dar es Salaam. Rais wa Tanzania, John Magufuli amemteua Dk John Ndunguru kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Ardhini (LATRA).

Taarifa iliyotolewa leo Jumatano Septemba 11, 2019 na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais Ikulu imemnukuu Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi John Kijazi ikisema uteuzi wa Dk Ndunguru umeanza Septemba 9, 2019.
Pia, taarifa hiyo imesema Rais Magufuli amemteua Profesa Antony Mshandete kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA).
Profesa Mshandete ni Naibu Makamu Mkuu wa Chuo (Taaluma, utafiti, ubunifu), Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST) kilichopo mkoani Arusha.
Imesema uteuzi huo umeanza Septemba 9, 2019.

Aliyekuwa Waziri wa uchukuzi awamu ya nne afariki dunia

Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Bodi ya kampuni ya simu za mkononi ya Airtel Tanzania, Dk Omary Nundu (71) amefariki dunia.

Taarifa iliyotolewa leo mchana Jumatano Septemba 11, 2019 na Kitengo cha Mawasiliano cha Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) Dar es Salaam kimesema, “Waziri wa zamani Omary Nundu alifikishwa leo MNH, akitokea nyumbani kwa gari binafsi la wagonjwa akiwa tayari ameshafariki.”
“Hivyo waliomleta waliamua wakahifadhi mwili wake katika hospitali ya rufaa ya Jeshi Lugalo,” imeeleza taarifa hiyo
Dk Nundu enzi za uhai wake aliwahi kuwa mbunge wa Tanga na Waziri wa Uchukuzi katika Serikali ya awamu ya nne  ya Tanzania.
Juni 12, 2019, Rais wa Tanzania, John Magufuli alimteua Dk Nundu kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Airtel Tanzania ikiwa ni utekelezaji wa makubaliano kati ya Serikali ya Tanzania na kampuni ya Bharti Airtel International.
Katika makubaliano hayo, Mwenyekiti wa Bodi ya Airtel Tanzania pamoja na ofisa mkuu wa ufundi wanapaswa kuteuliwa na Serikali.
Kabla ya Dk Nundu aliyezaliwa Agosti 6 mwaka 1948 kuteuliwa alikuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL)

Tuesday, September 10, 2019

Nape amuomba msamaha Rais Magufuli



Dar es Salaam. Rais wa Tanzania, John Magufuli amesema amemsamehe mbunge wa Mtama (CCM),  Nape Nnauye huku akielezea namna ambavyo mbunge huyo amekuwa akimuomba radhi.
Akizungumza Ikulu leo Jumanne Septemba 10, 2019 Rais Magufuli amesema kwa muda mrefu Nape amekuwa akimuomba msamaha kupitia ujumbe mfupi wa simu ya mkononi na kuwatumia baadhi ya wazee wa chama hicho tawala.
Rais Magufuli amesema Nape alifikia hatua ya kwenda kwa Makamu Mwenyekiti wa CCM, Philip Mangula, mjane wa Baba wa Taifa, Maria Nyerere pamoja na Mkurugenzi Mkuu mstaafu  wa Idara ya  usalama  wa Taifa nchini Tanzania, Apson Mwang'onda
“Alienda kwa mzee Mangula, amefika mpaka kwa Mzee Apson, Mama Nyerere amehangaika kweli lakini baadaye ni katika hiyohiyo sisi tumeumbwa kusamehe.”
“Leo nimemuona asubuhi amekuja hapa baadaye nikaona siwezi nikamzuia, ngoja niache shughuli zangu nimuone nilikuwa na kikao kingine kikubwa anachozungumza ninaomba baba unisamehe,” amesema Magufuli.
Kiongozi mkuu huyo wa nchi amesema, “Na mimi nimeshamsamehe tena kwa dhati kutoka moyoni mwangu, nimeshamsamehe na nimeshamsamehe kweli. Nape nenda ukafanye kazi, Mungu akujalie.”
 “Unamuona kabisa huyu mtu anaomba msamaha na leo kaniomba aje anione na saa nyingine  wasaidizi wangu wamekuwa wakipata hizo habari,” amesema Rais Magufuli
Awali, akizungumza Nape aliyewahi kuwa Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM amesema, “nimekuja kumuona (Magufuli) kama baba yangu, lakini mwenyekiti wa chama changu, Rais wangu kwa sababu wote mnajua mambo yaliyopita yalitokea ni mengi hapa katikati na mimi kama mtoto wa CCM mwanaye niliona ni vizuri nije niongee na baba yangu.”
“Kwa hiyo baada ya kupata fursa nimekuja nimemuona na mle ambamo nilimkosea kama baba yangu nimeongea naye na baba amenielewa, ameniambia amenisamehe na amenipa ushauri ambao nitaufanyia kazi na naamini baada ya hapa mambo yatakwenda vizuri.”
Mbunge huyo amesema, “kwa kweli kwa dhati ya moyo wangu nimshukuru sana sana, amenipa fursa kubwa, ndefu na ameongea maneno mengi kwangu na ushauri wake nimeuchukua.”
Ingawa si Nape wala Rais Magufuli waliozungumza hasa kwa nini wamekutana lakini katika siku za hivi karibuni kuliibuka sauti za viongozi mbalimbali wakiwamo za wabunge wa CCM, January Makamba (Bumbuli) na Willium Ngeleja (Sengerema) wakizungumzia suala la waraka ulioandika na makatibu wakuu wa CCM waliopita, Yusuf Makamba na  Abdurahman Kinana.
Wazee hao wa CCM waliandika  waraka huo kulalamikia mambo mbalimbali kwenda kwa Katibu wa Baraza la ushauri wa viongozi wa CCM, Pius Msekwa wakizungumzia mmoja wa   wanaharakati  ambaye amekuwa akiwachafua bila hatua kuchukuliwa.
Mpaka sasa bado haijafahamika kama hatua zimechukuliwa na hivi karibuni, Rais Magufuli alisema January na Ngeleja walikwenda kumwomba radhi kuhusu sauti hizo alizodai kuwa ni za kwao.
Nape ni miongoni mwa wanaotajwa kuhusika katika sauti hizo.

Monday, September 9, 2019

Mahakama yakataa maombi ya Lissu kupinga kuvuliwa ubunge

Mahakama Kuu,Tundu Lissu,mbunge wa Singida Mashariki, mwananchi habari,

Mawakili wa upande wa Tundu lissu
Dar es Salaam. Mahakama Kuu imekataa maombi ya aliyekuwa mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu kufungua shauri la maombi ya kutengua uamuzi wa Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai uliosababisha ubunge wake kukoma.
Imesema mwanasheria mkuu huyo wa Chadema hakupaswa kuwasilisha maombi hayo, alitakiwa kufungua kesi ya kupinga uchaguzi wa ubunge katika jimbo hilo.
Akisoma uamuzi huo wa mahakama leo Jumatatu Septemba 9, 2019 Jaji Sirillius Matupa amesema kama maombi yake yakikubaliwa yatasababisha uvunjaji wa katiba kwa kuwa italazimika kuwa na wabunge wawili kwenye jimbo moja.
Lissu alifungua maombi chini ya hati ya dharura, kupitia kwa kaka yake Alute  Mughwai ambaye amempa mamlaka ya kisheria kumwakilisha, ikiwa ni hatua ya awali kabisa ya kupigania kurudishiwa ubunge wake.
Katika maombi hayo namba 18 ya mwaka 2019, dhidi ya Spika wa Bunge na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Lissu aliomba kibali cha kufungua shauri kupinga taarifa ya Spika ya kukoma kwa ubunge wake na mahakama iteunge taarifa hiyo.Lissu yuko nchini Ubelgiji, kwa ajili ya matibabu baada ya kushambuliwa kwa risasi na watu ambao hadi sasa hawajajulikana, tangu Septemba 7, 2017, aliposhambuliwa, katika makazi yake, jijini Dodoma akitokea bungeni.
Juni 28, 2019, wakati akiahirisha mkutano wa 15 wa Bunge, Spika wa Bunge Job Ndugai alitangaza kukoma kwa ubunge wa Lissu, huku alijitetea kuwa si yeye aliyemvua ubunge bali ni matakwa ya Katiba ya Nchi.
Alitaja sababu za uamuzi huo kuwa ni kutokuhudhuria vikao vya bunge kwa muda mrefu bila kumjulisha Spika kwa maandishi mahali aliko na kutokuja taarifa za mali na madeni kwa mujibu wa Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.

Wednesday, September 4, 2019

Air Tanzania yaachiwa huru

Mahakama Kuu ya Gauteng, Johannesburg ,ndege ya Tanzania,mwananchi habari,


Dar es Salaam. Mahakama Kuu ya Gauteng, Johannesburg nchini Afrika Kusini imeiruhusu ndege ya Tanzania iliyokuwa imezuiwa katika uwanja wa ndege wa Oliver Tambo nchini humo kuondoka.
Ndege hiyo aina ya Airbus A220-300 ilizuiwa katika uwanja huo Agosti 23, 2019 kwa amri ya mahakama hiyo baada ya Hermanus Steyn kufungua kesi katika mahakama hiyo akidai fidia ya dola 33 milioni.
Akizungumza na Mwananchi kwa simu leo Jumatano Septemba 4,2019 kutoka Afrika Kusini, Naibu Waziri Mambo ya Nje ya Tanzania, Dk Damas Ndumbaro amesema Serikali ya Tanzania imeshinda kesi hiyo bila kutoa fedha yoyote ambayo aliyetushitaki alitaka Serikali ya Tanzania tuweke fedha kama dhamana dola milioni 33.
“Tumeshinda na ndege imeruhusu kuondoka. Kwa sasa hakuna kesi yoyote.”
“Sisi tulivyokuwa tunatukanwa kwenye mitandao tulikuwa tunaangalia tu, tulikuwa tunajua kazi tunayoifanya. Lazima ujue huku zimekuja PhD tatu,” amesema Dk Ndumbaro kutoka Afrika Kusini leo Jumatano.
Msemaji Mkuu wa Serikali ya Tanzania, Dk Hassan Abbas kupitia akaunti yake ya twitter ameandika, “Mahakama Kuu ya Gauteng, Afrika Kusini, leo imetoa hukumu na kuamuru kuwa ndege ya @AirTanzania iliyokuwa ikishikiliwa nchini humo iachiwe na mlalamikaji alipe gharama za kesi. Tunawashukuru wote kwa uvumilivu wenu.”

Monday, September 2, 2019

Rais Magufuli azungumza na watendaji wa kata nchi nzima

Rais  wa Tanzania, John Magufuli,kikao cha watendaji wa kata, mwananchi habari, habari mwananchi,

Dar es Salaam. Rais  wa Tanzania, John Magufuli amewataka watendaji  wa kata nchini kutoa taarifa kuhusu wakurugenzi, mawaziri  na wakuu wa mikoa wanaofanya matendo yanayokiuka misingi ya utawala bora.
Ametoa kauli hiyo leo Jumatatu Septemba 2, 2019 Ikulu jijini Dar es Salaam alipokutana na watendaji hao kutoka mikoa yote nchini.
Amebainisha kuwa mtendaji wa kata ndio bosi wa  eneo  lake, “Hata kama kuna kiongozi wa nafasi gani yuko chini yako na anapoonekana kuenenda visivyo unapaswa kumwajibisha au kutoa taarifa kwa mamlaka yake.”
“Katika kata kuna mkurugenzi wa halmashauri, RC (mkuu wa Mkoa), waziri au nani, wewe (mtendaji kata) ndio msimamizi, kama wewe upo katika kata na ambayo kuna waziri, RC, mkurugenzi  sijui  nani wewe ndiyo msimamizi,” amesema Magufuli.
Ameongeza, “Usiogope kumlima (barua) na kumwandikia maoni, hata kama anakuzidi cheo kwamba katika kata hii namwona mtumishi huyu anakwenda kinyume na maadili. Na ukimwona ni mkubwa sana, piga nakala hapa kwangu, lazima watu tujifunze kuogopana.”
Huku akizungumza zaidi kwa mifano amesema, “Kila siku anapigana (kiongozi) baa katika kata yako kwa sababu ni mkubwa unaacha kumripoti, chalaza kalamu na ndio maana watendaji kata wana kalamu na saini zao.”
Huku akiwataka kutokubali kudharaulika katika maeneo yao, Magufuli amesema, “Hapa (Ikulu) ni kwenu na mimi ni mpangaji tu hapa na mnaoamua nani aende Ikulu ni nyinyi na wananchi.”
“Hapa wamekaa hadi Wajerumani, amekaa  Nyerere (Julius) akaondoka, akaja Mwinyi (Ali Hassan) akaondoka, amekuja Mkapa (Benjamin) akaondoka, amekuja Kikwete (Jakaya)  akaondoka na mimi nitakaa na kuondoka,” amesema.
“Ndio maana sikusita kuwakaribisha , najua mko mahali pema salama na nilifikiri ni eneo hili tu tunaweza kukaa na kuzungumza vizuri. Nikija wilayani hawawasogezi karibu,” amesema.

Sunday, September 1, 2019

Mwendokasi lateketea lote kwa moto


Dar es Salaam. Basi la Kampuni ya Mwendo Haraka (Udart) maarufu 'Mwendokasi' lililokuwa likitoka Mjini kwenda Kimara Mwisho Dar es Salaam nchini Tanzania limeteketea lote kwa moto.


Tukio hilo limetokea leo usiku  wa Jumapili Septemba 1, 2019 eneo la Kimara Mwisho na kusababisha adha kwa watumiaji wa usafiri huo huku watu wengi wakijitokeza kushuhudia basi hilo ambalo limetekelea lote.

Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Teopista Malya amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kusema hakuna madhara kwa binadamu yaliyotokana na ajali hiyo.

Kamanda Malya amesema basi hilo lilitoka Mjini likiwa na abiria na lilipofika eneo la Kimara Mwisho walifanikiwa kushuka kabla halijateketea kwa moto.

Amesema Jeshi la Polisi linaendelea na kukusanya taarifa zaidi za ajali hiyo, ikiwemo hasara iliyosababishwa na ajali hiyo

Friday, August 30, 2019

Kilichojiri ndege ya Air Tanzania kukamatwa Afrika Kusini


Dar es Salaam. Jopo ya wanasheria waliopelekwa na Tanzania kupinga amri ya kushikiliwa kwa ndege ya Air Tanzania wameiambia mahakama ya Gauteng, Afrika Kusini kwamba amri ya kushikiliwa ndege hiyo ilitolewa kimakosa.
“Tumeonyesha kwamba amri ya kuishikilia ndege ya  Air Tanzania aina ya airbus A220-300 ilitolewa kimakosa dhidi ya Serikali, kwa hiyo tumetaka iondolewe,” wakili  Ngaukaitobi aliiambia mahakama.
Wakili Roger Wakefied anayemwakilisha mkulima Hermanus Steyn amesisitiza kuwa kuna kesi ya msingi ya kujibu na ameitaka mahakama hiyo kuangalia vigezo vya madai hayo na kuvitendea haki.
Kwa mujibu wa Wakefield hatua ya kwanza ya vigezo vya kesi hiyo vimeshathibitishwa.
Ndege hiyo ilishikiliwa Agosti 23, 2019 nchini humo kutokana na mvutano wa kisheria uliodumu kwa miongo kadhaa kati ya Serikali ya Tanzania na mkulima  Hermanus Steyn.
Mali za Steyn ikiwemo kampuni ya mbegu ya Rift Valley Seed Company Limited na mali nyinginezo zilitaifishwa na Serikali ya Tanzania Januari 1982. Amekuwa akiidai Serikali Sh373 milioni.
Hata hivyo, Julai 9, 2010 Jaji mstaafu Josephat Mackanja wa mahakama kuu alimpa Steyn tuzo ya Dola za Kimarekani 36,375,672.81.
Kuna ushahidi kuwa baada ya kutolewa kwa tuzo na Mahakama hiyo kulikuwa na makubaliano kati ya pande mbili yaliyoishusha hadi kufikia Dola 30 milioni na Serikali ya Tanzania ililipa kiasi kikubwa cha deni hilo kupunguza madai hayo.
Akizungumza na gazeti la Daily News, Wakili mkuu wa Serikali, Ally Possi amesema timu ya mawakili wanane kutoka ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali watapambana kwenye kesi hiyo iliyotajwa Agosti 21, 2019  ambayo hati ya dharura iliwekwa na kampuni ya mawakili ya Werksman’s Attorneys ikitaka ndege yoyote ya ATCL ili kufanikisha malipo ya tuzo hiyo.

Thursday, August 29, 2019

Rais Magufuli abainisha changamoto za umaskini Afrika

Rais John Magufuli wa Tanzania,Ikulu ya Dar es Salaam nchini Tanzania , Samia Suluhu,mwananchi, habari mwananchi,


Dar es Salaam. Rais John Magufuli wa Tanzania amesema masalia ya fikra za kikoloni walizonazo Waafrika wengi ni miongoni mwa sababu zinazofanya Bara la Afrika kushindwa kusimamia rasilimali zake ili kuleta mabadiliko ya kijamii na kiuchumi.
Ameyasema hayo jana Alhamisi Agosti 29,2019 Ikulu jijini Dar es Salaam alipokuwa akihutubia kongamano la viongozi la 2019 akisema dhana ya uhuru haiwezi kutenganishwa na kujitegemea.
“Kama hujitegemei huwezi kuwa huru, kwani uhuru wako utakuwa mikononi mwa unayemtegemea.”
“Maana hasa ya kupigania uhuru ni kurejesha rasilimali zetu na hasa rasilimali zetu, lakini pia kuwa na uamuzi kamili wa namna ya kuzisimamia na kuzitumia wa kuzitumia ili kuleta ukombozi wa kiuchumi,” amesema Rais Magufuli.  
Amesema kutokana na kutoelewa dhana kamili ya uhuru, nchi za Afrika zinadhani watawala wa zamani ndiyo wenye uwezo wa kusimamia na kusaidia na kuendeleza rasilimali.
Ametaja pia sababu ya kushindwa kusimamia rasilimali na kuleta mageuzi ya kiuchumi, akisema fedha siyo msingi wa rasilimali.  
“Fedha ni matokeo ya mwisho kabisa ya matumizi ya rasilimali zetu na siyo msingi wa maendeleo. Hata hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere alisema ili tuendelee tunahitaji watu, ardhi, siasa safi na uongozi bora. Hakutaja pesa, alijua itakuja tu kama yale tutayatimiza,” amesema.
Ametaja pia ukosefu wa ubunifu na teknolojia ya viwanda akisema Afrika haitaweza kusimamia na kutumia rasilimali zake kiuendelevu bila kuwa na viwanda.
Mbali na viwanda, ametaja kukithiri kwa migogoro na hali tete ya siasa barani Afrika akisema inasababishwa na mabeberu wanaotaka kuendelea kutumia maliasili za Afrika kwa manufaa yao.
“Wakati sisi tunapigana wao wanakula na kamwe hawatataka tuwe na amani, kwani migogoro ndiyo mtaji wao,” amesema.
Ameendelea kutaja pia tatizo la mikataba na makubaliano yanayoingiwa na wawekezaji katika kutumia rasilimali akisema, “Na hapa nchi yetu imeliwa sana kutokana na mikataba mibovu na hasa kwenye madini.”
Kuhusu uharibifu wa mazingira, Rais Magufuli amesema unasababishwa na ukataji hovyo wa msitu kwa ajili ya nishati ya majumbani kutokana na gharama kubwa za umeme na gesi asilia.  
“Chanzo kingine ni uchafuzi wa mazingira unaofanywa na mataifa mengine yaliyoendelea na yenye viwanda vingi, lakini Afrika ndiyo inayoathirika zaidi a machafuko hayo,” amesema.
Akizungumzia hatua zilizochukuliwa na Serikali, Rais Magufuli amesema imetungwa sheria ya kulinda utajiri na rasilimali na maliasili ya 2017 na kupitiwa upya na kurekebisha mikataba ya uchimbaji na madini isiyo na manufaa kwa Taifa.
“Tumeweka msukumo mkubwa kwenye ujenzi wa viwanda na ukuzaji wa teknolojia ya viwanda ili mazao yanayotokana na rasilimali zetu yasindikwe kwanza kabla ya kuuzwa nje,” amesema
Alitaja pia uanzishwaji wa mradi wa bwawa la Nyerere utakaozalisha MW 2115 kwenye bonde la mto Rufiji kama njia ya kutunza mazingira, kudhibiti nidhamu za watumishi wa umma na kupamba na rushwa na ufisadi.  
Wageni maarufu waliohudhuria mkutano huo walikuwa marais wastaafu kutoka baadhi ya nchi za Afrika akiwemo Thabo Mbeki wa Afrika Kusini, Olusegun Obasanjo wa Nigeria, Benjamin Mkapa na Jakaya Kikwete wa Tanzania.

Wednesday, August 28, 2019

Waziri mkuu ataka ATCL kuanza safari za mauritius

Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa,Shirika la Ndege la Tanzania,ATCL,

Dar es Salaam. Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amesema umefika wakati wa Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) kuanza safari za Mauritius ili kuvutia watalii zaidi.
Ametoa kauli hiyo leo Jumatano Agosti 28, 2019 alipokutana na waziri mkuu wa nchi hiyo, Pravind Kumar nchini Japan wakati akiwakaribisha wafanyabiashara wa Mauritius kuwekeza Tanzania.
Taarifa iliyotolewa na ofisi ya waziri mkuu leo inaeleza kuwa wafanyabiashara hao wanaweza kuwekeza katika uzalishaji wa sukari, uvuvi na kujenga viwanda vya nyuzi za pamba na nguo.
Majaliwa amesema kuanzishwa kwa safari za moja kwa moja kwenda Mauritius kutachangia kuwahamasisha watalii kuwekeza nchini.
“Umefika wakati wa ATCL kufikiria kuhusu safari za kwenda  Mauritius ili  kuwarahisishia wanaokwenda kufanya utalii wa fukwe  katika nchi hiyo inayofanya vizuri katika sekta hiyo na kwa sababu Tanzania ina fukwe za bahari na maziwa kupitia ushirikiano huo utatuletea tija,” amesema.
Naye Pravind ameihakikishia Tanzania kuwa nchi  hiyo ipo  tayari kufanya mazungumzo na wizara na taasisi zinazohusika na uwekezaji nchini.

“Tunataka kupata taarifa za kutosha zitakazotuwezesha kuwashawishi wafanyabiashara wa nchi yangu waje kuwekeza Tanzania.” Amesema Pravind

Sunday, August 25, 2019

Sababu ya Air Tanzania kuzuiwa Afrika kusini



Dar es Salaam. Serikali ya Tanzania imesema Mahakama Kuu nchini Afrika Kusini imezuia ndege ya Air Tanzania kuondoka nchini humo  kuanzia jana Jumamosi Agosti 24, 2019 kutokana na kesi ya madai iliyofunguliwa na Hermanus Steyn.
Steyn,  raia wa Afrika Kusini anadai fidia baada ya mali zake kutaifishwa na Serikali ya Tanzania mwaka 1980.
Hayo yameelezwa leo Jumapili Agosti 25, 2019 na msemaji wa Serikali ya Tanzania, Dk Hassan Abbas wakati akihojiwa na Shirika la Utangazaji nchini (TBC).
Ndege hiyo aina ya Airbus A220-300 imeshikiliwa katika uwanja wa Oliver Tambo jijini Johannesburg baada ya kufanya safari kadhaa tangu Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) lianze kufufua ruti zake za nje ya nchi.
Katika maelezo yake Dk Abbas amesema Steyn aliridhia mali hizo kutaifishwa lakini hoja ikaja alipwe fidia kiasi gani.
“Ndege zetu zipo salama kwa maana ya ndege sita ambazo Air Tanzania kwa sasa inaziendesha isipokuwa hii moja ambayo tumetoa taarifa kuwa imezuiwa kwa ajili ya kesi.”

“Watu wanahusisha jambo hili na madeni ya zamani kwenye shirika  kati ya Air Tanzania na Shirika la ndege Afrika ya Kusini. Niseme tu kuwa hii kesi haihusiani kabisa na hilo,” amesema Dk Abbas.
Ameongeza, “Alikuwa (Steyn) na mashamba, mifugo na mali nyingi kwa hiyo Serikali kwa wakati huo ikaona ni sahihi hizi mali zitaifishwe kwa hiyo ukitaka kuchimbua mgogoro huu asili yake unatoka miaka ya 1980.”
Amesema ilipofika miaka ya 1990 walikubaliana fidia atakayolipwa, miaka ya 2000 akalipwa na kuna kiasi kilichobaki ambacho mhusika amefungua kesi akitaka amaliziwe kulipwa.
“Ukiangalia awamu zote (za uongozi) kulikuwa na makubaliano, ukiangalia hatua za kimahakama wanakubaliana lakini malipo hayakufanywa lakini yalikuja kufanyika katika awamu ya nne,” amesema Dk Abbas.
Dk Abbas amesema mdai  huyo amekwenda Afrika Kusini kwa taratibu za mahakama, akibainisha kuwa zipo nchi ambazo mtu anaruhusiwa kuiomba hukumu ya nchi nyingine itekelezwe kwenye nchi aliyopo, akisisitiza kuwa ni  taratibu za kawaida kwenye sheria.
“Sisi tunaheshimu utawala wa sheria kwa sababu ni mfumo wa kawaida. Sheria itafuata mkondo wake, ukisoma ile hukumu inaturuhusu kuipinga.”
“Nafikiri  wanasheria wetu wataichambua na wataona hatua gani za kuchukua lakini ni mfumo wa kisheria ambao Serikali tunaufuata na tunauheshimu. Tunawahakikishia Watanzania kuwa tunasimamia maslahi ya Taifa,  ndege yetu itarudi na itaendelea na shughuli zake za kawaida,” amesema Dk Abbas.
Amesema kesi ya msingi haijasikilizwa kwa sababu anayedai fidia  ametumia sheria za Afrika Kusini kuomba kutekeleza hukumu ya nchi nyingine.
“Kesi ya msingi ya kiasi kilichobaki kwamba tukilipe haikusikilizwa, yeye aliomba maombi madogo ambayo pia yana sehemu mbili,  kusikilizwa wote (Serikali ya Tanzania na mdai) na mahakama au kusikilizwa yeye mwenyewe kama alivyofanya,” amesema Dk Abbas.

Friday, August 23, 2019

Air Tanzania yazuiwa kuruka na mahakama Afrika kusini



Dar es Salaam. Ndege ya Air Tanzania iliyokuwa inatoka Afrika Kusini kwenda jijini Dar es Salaam, Tanzania imezuiwa kuruka kwa amri ya Mahakama Kuu ya Gauteng, Johannesburg nchini humo.
Taarifa iliyotolewa jana Ijumaa   Agosti 23, 2019 na katibu mkuu Wizara ya Ujenzi,  Uchukuzi na Mawasiliano, Dk Leonard Chamuriho inaeleza kuwa Serikali ya Tanzania kupitia ofisi ya mwanasheria mkuu inafuatilia suala hilo ili ndege hiyo iachiwe na kuendelea na safari zake kama kawaida.
"Waziri wa Ujenzi,  Uchukuzi na Mawasiliano anaomba radhi kwa usumbufu uliojitokeza kwa abiria wa Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) waliokuwa wanasafiri leo kutoka uwanja wa ndege wa kimataifa wa Oliver Tambo,  Johannesburg kuja Dar es Salaam kufuatia ndege hiyo kushindwa kufanya safari kama ilivyopangwa, " inaeleza taarifa hiyo.
Inabainisha kuwa kwa mujibu wa taarifa ambazo Serikali imepokea kutoka kwa balozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini, ndege hiyo imezuiwa kwa amri ya mahakama hiyo.

Thursday, August 22, 2019

Rais Magufuli ataka mabalozi wajitathimini



Rais wa Tanzania, John Magufuli


Dar es Salaam. Mabalozi wa Tanzania wanaoiwakilisha katika nchi mbalimbali duniani wamempongeza Rais wa nchi hiyo, John Magufuli kwa utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati ambayo inajengwa kwa fedha za Watanzania.
Mabalozi hao 43 ambao wapo Tanzania tangu  Agosti 13, 2019 wametoa pongezi hizo leo Alhamisi Agosti,22, 2019 walipokutana na kuzungumza na Rais Magufuli Ikulu Jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya miradi waliyoitembelea mabalozi hao ni ujenzi wa bwawa la Nyerere litakalozalisha megawati 2,115 katika mto Rufiji, ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kisasa, jengo la tatu la abiria katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Julius Nyerere na ujenzi wa barabara za juu katika makutano ya barabara ya Morogoro na Sam Nojuma.
Pia, walitembelea Zanzibar katika ujenzi wa jengo la biashara na makazi (shopping mall) eneo la Michenzani, ujenzi wa jengo la tatu la abiria katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Sheikh Abeid Amani Karume, ujenzi wa nyumba za kisasa wa Fumba Wilaya ya Magharibi na ujenzi wa barabara ya Kaskazini - Bububu – Mkokotoni .
Mabalozi hao wameeleza utekelezaji wa miradi hiyo pamoja na juhudi nyingine kubwa zinazofanywa na Serikali ya Tanzania katika nyanja mbalimbali za huduma za jamii zimeleta heshima kwa nchi na machoni mwa Jumuiya ya Kimataifa na kwamba zimedhihirisha kufikiwa kwa malengo ya Tanzania kuingia katika uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.
Akizungumza baada ya kuwasikiliza Mabalozi hao, Rais Magufuli amewapongeza kwa kazi wanazozifanya katika nchi wanazoiwakilisha nchi na amewataka waendelee kutekeleza majukumu yao kizalendo na kwa kutanguliza maslahi ya Tanzania.

Pamoja na kueleza kuhusu hali ya uchumi wa nchi, juhudi za kuwapelekea maendeleo Watanzania na juhudi za kujenga uwezo wa kujitegemea, Rais Magufuli amewataka Mabalozi hao kutafuta wawekezaji watakaowekeza katika miradi yenye manufaa hapa nchini.
“Nataka Mabalozi mtuletee miradi ya maendeleo, ifike mahali Balozi ujiulize kwa kuwa kwangu Balozi nimepeleka nini nyumbani? Nimewezesha kujengwa kiwanda? Kujengwa barabara? Kujenga daraja au jengo fulani?” amesema Rais Magufuli ambaye pia ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (Sadc)
Rais Magufuli amewasisitiza Mabalozi hao kuhakikisha wanasimamia na kufuatilia kwa karibu masuala wanayoamini yana manufaa kwa nchi ikiwemo uwekezaji na kwamba wasikubali kukwamishwa na viongozi ama wizara yoyote.
“Nataka muwe very aggressive, na ukiona mtu anakukwamisha mimi nipo niandikieni uone kama hatakwama yeye, mimi nataka kuona vitu sio maneno maneno” amesisitiza Rais Magufuli.
Kuhusu changamoto mbalimbali walizomueleza, Rais Magufuli ametoa wito kwa Mabalozi hao kuzishughulikia pale ambapo wao wenyewe wana uwezo na amemtaka Wizara ya Mambo ya Nje, Profesa Palamagamba Kabudi kufanyia kazi taarifa wanazopelekewa na Mabalozi  hao kwa wakati.

Wednesday, August 21, 2019

Tanzania Kukopeshwa sh.3.9 Trilioni na Benki ya Dunia



Dar es Salaam.  Benki ya Dunia (WB) imesema ipo tayari kuipaTanzania mkopo wa masharti nafuu wa Dola 1.7 bilioni ambazo ni zaidi ya Sh3.9 trilioni.
Fedha hizo ni zile zilizobaki katika fungu awamu ya 18 ya mgao wa chama cha kimataifa cha maendeleo (IDA) kilichopo ndani ya WB ambacho hujihusisha na kuzisaidia nchi masikini zaidi duniani kupambana na umasikini.
Leo Jumatano Agosti 21, 2019 mkurugenzi mtendaji wa WB anayesimamia nchi 22 zilizoko Kanda ya Afrika, Anne Kabagambe amemueleza Waziri wa Fedha na Mipango wa Tanzania, Dk Philip Mpango kuwa kiasi hicho cha fedha kinatarajiwa kutolewa kabla ya kuanza mgao mpya wa 19 wa IDA utakaoanza Julai 2020.
Kabagambe ambaye yupo nchini kwa  ziara ya kikazi amesema fedha hizo zitatolewa mara baada ya kukamilisha taratibu zote za upatikanaji wake.
”Fedha hizi zitaelekezwa katika kutekeleza miradi kadhaa muhimu ikiwemo ya elimu, afya, mradi wa kusaidia kaya masikini kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (Tasaf) awamu ya pili na uendelezaji wa miji na masuala ya uchumi jumuishi  Zanzibar,” amesema Kabagambe
Taarifa iliyotolewa na wizara ya fedha imeeleza  Kabagambe amepongeza hatua zinazochukuliwa na Serikali ya Tanzania katika kupiga vita rushwa na ufisadi pamoja na kutekeleza miradi ya jamii ikiwemo reli na kufua umeme.

Kwa upande wake, Dk Mpango ameiomba benki hiyo kuisaidia Serikali kwa kuipatia fedha za kufanikisha ujenzi wa miundombinu hiyo ya umeme, reli, maji safi na salama, kuimarisha sekta ya kilimo, viwanda, bandari, rasilimali watu na masuala ya teknolojia ya habari na mawasiliano.
Amesema miradi hiyo itachochea zaidi ukuaji wa uchumi na kupunguza umasikini wa wananchi kwa kuwa nishati ya umeme itachochea ukuaji wa sekta ya viwanda hivyo na kukuza ajira, na reli itaimarisha sekta ya usafiri na uchukuzi.

Tuesday, August 20, 2019

Ajari ya moto Morogoro waliofariki wafikia 99


  • Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Morogoro (RC) nchini Tanzania, Dk Stephen Kebwe amesema vifo vinavyotokana na ajali ya lori la mafuta ya petroli kuanguka kisha kuwaka moto imefikia 99 baada ya majeruhi wawili kufariki dunia.
Majeruhi hao waliofariki ni kati ya 18 waliokuwa wamelazwa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Dar es Salaam katika chumba cha uangalizi maalum (ICU).
Akizungumza na Mwananchi kwa simu leo jioni Jumanne Agosti 20,2019, Dk Kebwe amesema, “Kwa taarifa ambazo tumezipata kutoka Muhimbili hadi leo saa 10 jioni, majeruhi wawili kati ya 18 wamefariki dunia na kufikisha idadi ya vifo 99.”
“Kwa maana hiyo kwa sasa kuna majeruhi 16 huku Morogoro na 16 Muhimbili wakiendelea na matibabu,” ameongeza mkuu huyo wa mkoa.
Ajali hiyo ya lori ilitokea asubuhi ya Jumamosi Agosti 10, 2019 eneo la Msamvu mkoani Morogoro baada ya kuanguka kisha kulipuka.

Monday, August 19, 2019

Uchaguzi Serikali za Mitaa waziri Jafo atoa tamko

Image result for jafo


Dar es Salaam. Serikali ya Tanzania imesema inatarajiwa kutangazwa tarehe maalum ya kufanyika kwa uchaguzi wa serikali za mitaa huku kampeni za uchaguzi huo zikifanyika kwa siku saba kabla ya siku ya uchaguzi.
Pia, uandikishwaji wa wapiga kura kwa ajili ya uchaguzi huo utafanyika siku 47 kabla ya uchaguzi.
Hayo yalisemwa jana Jumatatu Agosti 19,2019 na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Suleimani Jaffo katika mahojiano maalumu na Kituo cha Televisheni cha Azam.
Alisema kutakuwa na tukio rasmi la kutangaza tarehe ya uchaguzi ambayo pia itaenda sambamba na ugawaji wa kanuni zitakazosimamia uchaguzi.
“Hakuna mtu anayejua tarehe ya uchaguzi, japokuwa vyama vyote vya siasa vilivyosajiliwa vilishiriki katika uandaaji wa kanuni, katibu tawala, asasi za kiraia, wakuu wa wilaya na mikoa,” alisema Waziri Jafo
Akizungumzia kujiandikisha alisema licha ya kufanyika kwa uchaguzi kama huo mwaka 2014 na watu kujiandikisha lakini hawatakuwa na sifa ya kupiga kura mwaka 2019.

“Kutakuwa na daftari jipya, kila kanuni inakuja na daftari lake, watu watajiandikisha katika mitaa yao na itakuwa ni siku 47 kabla ya.”
“Na kabla ya uchaguzi, kutakuwa na siku saba za kampeni na kwa serikali za mitaa ni nyingi sana kwa sababu siku moja wanaweza kumaliza mitaa yote na kwa hizo siku tulizotoa si ajabu wakapita nyumba kwa nyumba,” alisema Jaffo.

Air Tanzania yatumika kumrudisha wazari mkuu wa Eswatini



Dar es Salaam. Waziri Mkuu wa Eswatini, Sibussiso Dhlamini ameondoka  jijini Dar es Salaam, Tanzania leo Jumatatu Agosti 19, 2019 kurejea katika nchi hiyo kwa kutumia ndege ya Shirika la Ndege Tanzania (ATCL).
Ameondoka leo mchana na  ndege aina ya Airbus A220-300 kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) huku akisindikizwa na Waziri wa Maji, Profesa Makame Mbarawa.
Dhlamini alikuwa nchini Tanzania kuhudhuria mkutano wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (Sadc) uliomalizika jana Jumapili.

Magufuli sasa ahamishia nguvu SADC



Dar es Salaam. Mwenyekiti mpya wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (Sadc), Rais John Magufuli amehamishia dhamira yake ya kutaka kuwapo kwa kasi ya maendeleo nchini katika jumuiya hiyo.
Katika hotuba yake ya kwanza mara baada ya kukabidhiwa wadhifa huo jana, Rais Magufuli alianza kwa kuishukia Sekretarieti ya Jumuiya hiyo akisema imeshindwa kuzishauri nchi wanachama namna ya kuondokana na mkwamo wa kiuchumi.
Tangu alipoingia madarakani mwaka 2015, Rais Magufuli amekuwa akisisitiza utendaji kazi usiokuwa wa mazoea, kujituma ili kuwasaidia wananchi hasa wanyonge kujikwamua kuichumi.
“Sisi siyo maskini,” alisema Rais Magufuli jana katika hotuba yake baada ya kukabidhiwa rasmi wadhifa huo na mtangulizi wake, Rais Hage Geingob wa Namibia.
Huku akitumia takwimu, mwenyekiti huyo mpya alitoa takwimu za miaka 10 kuonyesha namna gani ukuaji wa kiuchumi ulivyo wa kusuasua huku sekretarieti ikishindwa kutoa majibu au hata kuzishauri nchi wanachama namna ya kuvuka vikwazo vya kiuchumi.
Alisema takwimu za ukuaji wa uchumi kwa nchi za Sadc haujawahi kufika asilimia tano na kwamba mara ya mwisho ilikuwa mwaka 2008 ambako ulikuwa kwa asilimia 5.7 na kusema sekretarieti hiyo imeonyesha upungufu katika utendaji wake.

Huku akishangiliwa na wajumbe waliohudhuria mkutano huo wa ufunguzi uliofanyika katika ukumbi wa Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere, mwenyekiti huyo alisema; “nchi zetu siyo maskini. Tuna rasilimali zote zinazoweza kutuondoa kwenye umaskini.”