
Dar es Salaam. Mahakama Kuu ya Gauteng, Johannesburg nchini Afrika Kusini imeiruhusu ndege ya Tanzania iliyokuwa imezuiwa katika uwanja wa ndege wa Oliver Tambo nchini humo kuondoka.
Ndege hiyo aina ya Airbus A220-300 ilizuiwa katika uwanja huo Agosti 23, 2019 kwa amri ya mahakama hiyo baada ya Hermanus Steyn kufungua kesi katika mahakama hiyo akidai fidia ya dola 33 milioni.
Akizungumza na Mwananchi kwa simu leo Jumatano Septemba 4,2019 kutoka Afrika Kusini, Naibu Waziri Mambo ya Nje ya Tanzania, Dk Damas Ndumbaro amesema Serikali ya Tanzania imeshinda kesi hiyo bila kutoa fedha yoyote ambayo aliyetushitaki alitaka Serikali ya Tanzania tuweke fedha kama dhamana dola milioni 33.
“Tumeshinda na ndege imeruhusu kuondoka. Kwa sasa hakuna kesi yoyote.”
“Sisi tulivyokuwa tunatukanwa kwenye mitandao tulikuwa tunaangalia tu, tulikuwa tunajua kazi tunayoifanya. Lazima ujue huku zimekuja PhD tatu,” amesema Dk Ndumbaro kutoka Afrika Kusini leo Jumatano.
Msemaji Mkuu wa Serikali ya Tanzania, Dk Hassan Abbas kupitia akaunti yake ya twitter ameandika, “Mahakama Kuu ya Gauteng, Afrika Kusini, leo imetoa hukumu na kuamuru kuwa ndege ya @AirTanzania iliyokuwa ikishikiliwa nchini humo iachiwe na mlalamikaji alipe gharama za kesi. Tunawashukuru wote kwa uvumilivu wenu.”
No comments:
Post a Comment